Tuesday, July 24, 2012


Rais Kikwete Akutana Na Dkt. Asha Rose Migiro

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika mazungumzo na aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa Dkt.Asha Rose Migiro ikulu jijini Dar es Salaam leo 


Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akimkaribisha na kufanya mazungumzo na aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa Dkt.Asha Rose Migiro ikulu jijini Dar es Salaam leo asubuhi

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akumuaga aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa Dkt.Asha Rose Migiro ikulu jijini Dar es Salaam leo. Chanzo: Freddy Maro

Mabasi ya Dar Express, Simba Mtoto yamegongana uso kwa uso eneo la Wami

Basi la Dar Express lililokuwa linatoka Arusha na basi la Simba Mtoto lililokuwa linaenda Tanga yamegongana uso kwa uso maeneo ya Wami. Mwanahabari wa "Globu ya Jamii" aliyekuwa eneo la tukio muda mfupi baada ya ajali kutokea anasema hadi anaondoka mahali hapo hakuna maafa ya watu kupoteza uhai yaliyoropotiwa ila, watu kadhaa wamejeruhiwa na kuna mtu mmoja amebanwa katikati ya mabasi ambayo kisa cha kugongana kwake bado hakijafahamika.

Majeruhi wa ajali hiyo wamepelekwa katika hospitali ya Chalinze.
Picture
Abiria wa wakishushwa kupitia madirishani
Picture
Abiria wakijaribu kumwokoa mwenzao aliyenaswa
Picture
Abiria wakiendelea na juhudi za kuwatoa wenzao

Maiti Mv Skagit zafikia 89



Idadi ya maiti za ajali ya kuzama kwa Meli ya MV Skagit zimeongezeka na kufikia 89 baada ya miili mingine 11 kupatikana leo katika maeneo manne tofauti ya  visiwa vidogovidogo vilivypo mwambao wa Zanzibar.

Afisa Habari Mkuu wa Jeshi la Polisi Zanzibar Inspekta Mohammed Mhina, amesema kuwa miili iliyopatikana leo, sita ni wanaume akiwemo kijana mdogo na mingine mitatu ya wanawake.
Inspekta Mhina amesema, maiti zote zimezikwa katika makaburi ya pamoja ya Kama yaliyopo nje kidogo ya mji wa Zanzibar chini ya usimamizi wa Jeshi la la Wananchi wa Tanzanaia JWTZ, Jeshi la Polisi, MKMK, JKU na Varantia.

Amesema miili hiyo ilipatikana katika viisiwa vya Pungume, Fumba, Chumbe na eneo linalokupwa na kujaa maji la Funguyasini maeneo jirani na kisiwa mama cha Unguja.

Naye Mkuu wa Polisi Kikosi cha Wanamaji na Bandari Zanzibar SP Martin Lisu, amesema kuwa kunauwezekano mkubwa kuwa maiti hizo zinaibuka kutoka katika meli hiyo ya Skagit.

Kamanda Lisu, amesema kuwa kutokana na kuendelea kuibuka kwa maiti hizo, Maafisa wa vyombo vya Ulinzi na Usalama wanaendelea na zoezi lao la kutafuta miili mingine na kupokea taarifa za kuonekana kwa mwili kutoka kwa watu wenye vyombo binafsi vya uvuvi na kuzifuatilia.

Hivi karibuni akizungumza na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete, Daktari Mkuu Mwelekezi wa Jeshi la Polisi nchini Dk. Ahamed Makata, alisema kuwa maiti nyungi zitaweza kupatikana ifikapo siku ya nne tangu kuzama kwa meli hiyo.

Alisema tabia ya maiti ya binadamu aliyekufa maji na kuzama, haiwezi kukaa chini ya maji kwa muda mrefu kama haikufungwa na kitu kizito kabla ya kuzama.

"Kwa kawaida maiti ya mtu aliyekufa maji haiwezi kukaa ndani ya maji wakati wote na kwamba hata kama itaendelea kubaki majini lakini katika muda wa kuanzia siku tatu na nne mwili ama miili hiyo nilazima ianze kuibuka na kuelea juu ya maji". Alisema Dk. Makata.

Sunday, July 22, 2012




 Magazetini Jumapili Hii july 22,2012











TATIZO LA MAJI LAWA KERO KWA WANANCHI WA NDULI MANISPAA YA IRINGA MJINI,AHADI ZA SERIKALI BUBU BAADA YA UCHAGUZI ZAWAACHA SOLEMBA BILI KUJUA CHA KUFANYA
Mwananchi wa Nduli akuzungumzia tatizo la maji Nduli


Mkazi wa Nduli katika huzuni ya kukosa maji Nduli
Mchoma nyama za mbuzi katika n=misitu ya katika kata ya kising'a Ismani Iringa

UGOMVI ULIOKUWA UKIHUSISHA PANDE MBILI ZA FAMILIA YA MAREHEMU WASULUHISHWA MKOANI MBEYA,.


 Sehemu ya mabati 57 yaliyotolewa na Familia ya Mligula iliyokuwa ikigombea mali za marehemu Eva Emmanual Mligula na Emmanuel Mwaigaga na kutoa vitisho kwa njia ya mtandao kwa Bwana Allan Mwaigaga,ambaye aliitaka familia hiyo kuchangia maendeleo ya Shule tatu za Msingi ya Itewe,Pankumbi na Mwashoma.
Viongozi wa kikabila(Machifu) na wanafamilia wa pande zote mbili za marehemu wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kumaliza tofauti zao.(Picha na Ezekiel Kamanga)
*******
Habari na Ezekiel Kamanga,Mbeya.
Ugomvi wa kugombea mali za marehemu uliokuwa unahusisha familia mbili za marehemu Eva Emmanuel Mligula(38) na Emmanuel Mwaigaga aliyefariki miaka nane iliyopita waliokuwa wakiishi Mtaa wa Utukuyu,Kata ya Uyole Jijini Mbeya umesuluhishwa baada ya familia hizo kukutanishwa na uongozi wa kimila na Serikali.
Awali ugomvi ulianza Julai 13 mwaka huu katika mazishi ya Mjane Eva,kufuatia Baba na kaka wa marehemu huyo kuwazuia ukoo wa Mwaigaga(kiumeni) kutokuwepo katika msiba na kutohudhuria mazishi kwa kile kilichodaiwa kuwa ukoo unaweza kuuza nyumba ya marehemu.
Mvutano huo ulielekea ukoo wa marehemu kubeba kila kitu kilichokuwemo ndani zikiwemo samani kwa kutumia gari yenye nambari T 788 BLK aina ya Fuso na T 314 AVA aina ya Center na kusababisha Bwana Allan Mwaigaga(Mwaji Group) kutoka ukoo unaotuhumiwa kutoa taarifa Kituo cha Polisi cha Uyole.
 Mkuu wa kituo hicho cha polisi Lazaro Kiyeyeu alifika eneo la tukio na kushuhudia vyombo vikibebwa na ukoo wa Mligula naye kwa kushirikiana  na Mwenyekiti wa mtaa Bwana Michael Mwamahondya kuchukua jukumu la kumtaarifu Diwani wa kata ya Uyole Bwana Ngambi Ngela ambaye aliwasihi wananchi waliokuwepo msibani hapo kurudi makwao na hivyo na kila familia ya marehemu kwenda kulilia msiba nyumbani kwao na nyumba hiyo ya marehemu kufungwa na yeye kukabidhiwa funguo kukabidhiwa Bwana Mwaigaga.
Aidha .baada ya funguo hizo kukabidhiwa hali ikawa tofauti kutokana na ukoo wa Mligula kuporomosha matusi na vitisho kwa Bwana Mwaigaga,ambaye alitoa taarifa Polisi na kufunguliwa kesi mbili dhidi ya ukoo huo,ambapo kesi ya kwanza yenye nambari MB/IR/57/67/2012  ya kutishia kuua kupitia njia ya mtandao na kesi ya pili ya Jinai 551/2012 ya kutoa kashifa mbele ya umma na kupora mali za marehemu.
Mnamo Julai 19,mwaka huu Katibu wa mila wa kabila la Kisafwa Chifu Mwalwego alipokea ombi la msamaha kutoka kwa familia ya Mligula kuomba wapatanishwe na ukoo wa Mwaigaga,baada ya kugundua wamefanya makosa ya kuchukua mali za marehemu badala ya kuziacha katika nyumba hiyo ambapo marehemu wameacha watoto watatu wawili wa kiume na mmoja wa kike ambao walipaswa kuacha mali hizo.
 Baada ya kupokea ombi hilo Chifu huyo aliwasiliana na Bwana Mwaigaga ambaye alikubali kusamehe na kutaka akutanishwe na ukoo huo Julai 21 mwaka huu majira ya saa nne katika eneo la nyumba ya marehemu iliyopo mtaa wa Utukuyu na kwamba yeye hataki kulipwa fidia yoyote licha ya kudharirishwa lakini ameutaka ukoo huo uchangie maendeleo katika shule tatu za msingi zinazozunguka eneo hilo ambazo ni Shule ya Msingi Itewe ipewe mabati 19 ya gauge 30 na shilingi 100,000 kwa Chifu wa mtaa huo.
Ameongeza kuwa Shule ya Msingi Pankumbi ipewe mabati 19 na shilingi 100,000 kwa chifu wa eneo hilo na Shule ya msingi Mwashoma ipewe mabati 19 na  shilingi 100,000 na Chifu Mwanshinga apewe shilingi 200,000 kama msuluhishi wa mgogoro huo.
Hata hivyo Julai 21 mwaka huu ukoo wa Mligula,ulilipa shilingi 500,000 na mabati 57 mbele ya uongozi wa Machifu na uongozi wa Kata ya Uyole baada ya kukutanishwa na ukoo wa Mwaigaga.
Kwa upande wake Bwana Allan Mwaigaga alisema hana kinyongo na kuahidi kufuta kesi mahakamani lakini pande zote mbili za familia zishirikiane kuwalea watoto hao walioachwa na marehemu,pia mali zituzwe na nyumba ipangishwe ili pesa zitumike kwa ajili ya kuwasomesha watoto kwani kwa kufanya hivyo iwe fundisho kwa watu wote wenye tabia za kuhodhi mali za marehemu na kuacha watoto wakihangaika.

TUKIO LA WANAFAMILIA KUGOMBANIA MALI ZA MAREHEMU.

Sehemu ya samani iliyokuwa ikimilikiwa na marehemu Eva Emmanuel Mligula na Emmanuel Mwaigaga,iliyogombaniwa na ndugu zikiwa zimetolewa nje kwa lengo la kuhamishwa katika Mtaa wa Utukuyu,Kata ya Uyole Jijini Mbeya.
 Baba Mzazi na Kaka wa marehemu Eva wakiwa nje ya nyumba iliyokuwa ikimilikiwa na  marehemu Eva Emmanuel Mligula na Emmanuel Mwaigaga katika Mtaa huo nayo iliingizwa katika mgogoro wa kugombaniwa,hali iliyopelekea Serikali kuingilia kati..
 Baadhi ya waombolezaji wakishuhudia tukio la kutolewa kwa vyombo vya marehemu vilivyokuwa vikigombaniwa na wanandugu.
 Mama mzazi wa marehemu Eva,anayefahamika kwa jina la Bi. Magreth Mzegeza(70) aliyevalia nguo nyeupe akiwa na baadhi ya waombolezaji.
 Moja ya magari yaliyotumika kuhamishia shehena ya mali za marehemu.
Sehemu ya Sebule ikiwa tupu baada ya vyombo vyote kubebwa na Kijana huyu alikuwa mstari wa mbele katika kuvitoa vyombo vya marehemu.(Picha na Ezekiel Kamanga,Mbeya).

Friday, July 20, 2012


 Ikiwa Serikali itazungumzia kilimo kwanza halafu tukawekeza katika maeneo yenye mti kama hii tutapata kitu

Miti hii kwa mikoa ya nyanda za juukusini hutumika kama zao la kinywaji kinacho tambulika kwa jina la Ulanzi ambacho ndicho kinywaji na kilevi kinachopendwa na watu wengi si wazee wala vijana wa mikoa hii ya nyanda za juu kusini

Inasadikika Ili ukosane na wakazi wa maeneo hayo jaribu kumshawishi akate miti hii na aache shughuli za ugemaji wa kinywaji hicho ambacho ndicho kinacho sababisha uvivu katika jamii za mikoa hiyo ambao hutumia muda mwingi kujihusisha na ugemaji na unywaji wa kinywaji hiki hususani muda wa kazi,kama hiyo haitoshi miti hii inaathari kwa mazao ya chakula kama mahindi kutokana na chumvichumvi inayotokana na mimea hii,

jamii nyingi za Ukanda huu huchanganya miti hii na mazao hali ambayo imechangia kwa kiasi kikubwa upungufu wa chakula katika maeneo yanayolimwa mianzi hii,

Je,tuwashauri nini ndugu zetu hawa wanaoumia kwa njaa na kupoteza muda mwingi kwa kukaa na kupoteza muda kwa ulevi?

''angalia picha ya mazao ya mahindi na mihogo hapo chini...............

Mianzi mti wa Ulanzi


Hii ni sehemu ya mji wa Ipogolo Manispaa ya Iringa Mjini

 

Serikali ya Tanzania inamtafuta nyoka wake mwenye umri wa miaka 209

 
Serikali imedhamiria kumsaka nyoka mwenye umri wa miaka 209 aliyepo katika Msitu wa Akiba Minziro, uliopo Wilaya ya Misenyi, mkoani Kagera.

Lengo la kumsaka nyoka huyo ni kutokana na ukongwe wake hivyo kuwa kivutio kikubwa duniani hasa katika sekta ya utalii.

Mkurugenzi wa Misitu na Nyuki nchini, Dkt. Felician Kilahama, aliyasema hayo juzi wakati akizungumza na waandishi wa habari. Akasema nyoka huyo mwenye futi 47, atapatikana baada ya mapito yake katika msitu huo kuonekana ila ni vigumu kuonekana hadharani kwa sababu hupendelea kuishi mapangoni, “Huyu nyoka lazima tumfanyie mahesabu ya kumkamata kirahisi, umri wa miaka 209 sio mchezo, ameweza kutambulika Baada ya kupima urefu wa mapito yake, pia kuna chatu na nyoka wenye mapembe,” alisema Dkt. Kilahama.

Aliongeza kuwa, licha ya nyoka kuhatarisha maisha ya watafiti lazima kufanyike uharaka wa kuupandisha hadhi msitu huo uwe hifadhi ya Taifa ili kuboresha usimamizi wake, “Kikao cha Kamati ya Ushauri cha Mkoa Kagera (RCC), kilipitisha msitu huu upandishwe hadhi, nyoka huyu ambaye ni aina ya Giant Forest Cobra, kichwa chake kina rangi nyekundu na sehemu ya kiwiliwili rangi ya kijani. Alianza kufanyiwa utafiti mwaka 2000 baada ya kupatikana kwa taarifa kutoka kwa wenyeji wa maeneo hayo juu ya kuwepo kwa aina ya nyoka huyo katika msitu huu,” alisema.

Kutokana na hali hiyo, uongozi wa Halmashauri ya Missenyi, kupitia Maofisa wa Misitu, mwaka 2010 walianza kuweka mitego ya sindano katika mapito anayotumia ili kuchukua damu yake na kwenda kuipima vina saba ndipo ilibainika kuwa hadi kufikia mwaka huo, alikuwa na miaka zaidi ya 207.

Dkt. Kilahama alisema nyoka huyo atakuwa kivutio muhimu mkoani hapa kama atapatikana licha ya kukabiliwa na tatizo la ukumbwa wa msitu ambao hekta 25,000 kwani nyoka huyo amekuwa akihama mara kwa mara kwa ajili ya mawindo.

Ofisa Misitu wilayani hapa, Bw. Wilbard Bayona, alisema nyoka huyo ana uwezo wa kuishi siku 68 bila kula chochote zaidi ya maji baada ya kumeza mnyama yeyote ambaye atamkamata mawindoni.

---
Theonestina Juma, 
Bukoba, Majira

 
Picture
Mkazi wa jiji alikutwa na kamera yetu akining'inia kwenye daladala lifanyalo safari kati ya Mwenge na Gongolamboto, bila kujali usalama wake, kama alivyokutwa eneo la Ilala Boma, Barabara ya Kawawa Dar es Salaam jana. (Picha na Charles Lucas) Mkazi wa jiji alikutwa na kamera yetu akining'inia kwenye daladala lifanyalo safari kati ya Mwenge na Gongolamboto, bila kujali usalama wake, kama alivyokutwa eneo la Ilala Boma, Barabara ya Kawawa Dar es Salaam jana.

Thursday, July 19, 2012



Maiti wa ajali ya MV Skagit watambuliwa; Wasiotambuliwa wamezikwa na Serikali


Baadhi ya miili ya maiti ya waliookolewa kutoka katika MV Skagit iliyozama hapo jana, wakitambuliwa na ndugu zao katika Viwanja vya Maisara Mjini Zanzibar, na kuruhusiwa kuichukuwa kwa ajili ya taratibu za mazishi. 
Balozi wa Marekani Nchini Tanzania, Lenhardt Alfonso wakatikati akionekana na huzuni Baada ya kuziona Maiti zilizookolewa katika Meli iliozama hapo jana katika Bahari ya Chumbe Zanzibar.Balozi alifika katika Viwanja vya Maisara ili kuona namna shughuli za kushughulikia maiti zinavyoendelea. 
Mama alietambulika kwa Jina la Bitatu Uyelo ambae amenusurika na kupoteza mtoto wake wa miezi tisa katika ajali ya MV Skagit. 


Waziri wa Mambo ya ndani wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Emanuel Nchimbi alifika katika eneo lililohifadhiwa Maiti wa ajali ya MV Skagit ili kutambuliwa na ndugu zao na kupata maelezo kwa Daktari Kiongozi (hayupo pichani) katika Viwanja Vya Maisara Zanzibar. 
Baadhi ya Maiti waliookolewa kutoka katika MV Skagit na kukosa watu wake, wakipelekwa kuzikwa na Serikali katika Eneo la Kama lililotayarishwa makusudi kwa ajili hiyo. 
----
[Picha na maelezo: Yussuf Simai - Maelezo via ZanziNews blog]

 
 

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimfariji mmoja wa walionusurika katika ajali ya meli jana huko Chumbwe wakati Rais na Mama Salma Kikwete walipowatembelea kuwafariji na kuwapa pole katika hospitali kuu ya Mnazi Mmoja leo Julai 19, 2012.


Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Mama Salma Kikwete wakitembelea Uwanja wa Maisara, Zanzibar, ambako ndiko miili ya marehemu huletwa kwa utambuzi baada ya kuokolewa kwenye eneo la ajali leo Julai 19, 2012.


Rais Jakaya Kikwete na Mama Salma Kikwete wakimsikiliza mmoja wa walionusurika katika ajali ya meli jana Bw Kitwana Makama Haji ambaye kalazwa katika hospitali kuu ya Mnazi Mmoja leo Julai 19, 2012 




Rais Jakaya Kikwete na Mama Salma Kikwete wakimpa pole Bi Salome Abeli, mmoja wa walionusurika katika ajali hiyo ya meli. Yeye ni mfanyakazi wa Tanzania Automic Energy Commission akitokea Arusha kwenda Pemba Kikazi leo Julai 19, 2012. 






PICHA: IKULU


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akisikiliza maelezo kutoka kwa Kadhi Mkuu wa Zanzibar, Khamis Haji Khamis, jinsi ulivyandaliwa utaratibu wa kuwahifadhi marehemu watakaokosa kutambuliwa na ndugu zao, wakati Makamu alipofika kwenye Viwanja vya Maisara mjini Zanzibar, leo Julai 19, 2012, kuangalia shughuli za uokoaji na utambuzi wa marehemu. Kushoto ni Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Muungano, Samia Suluhu Hassan.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akimsikiliza mmoja kati ya vijana walionusulika katika ajali ya Meli ya Skagit, Kitwana Makame Ali (24) mkazi wa Unguja, wakati alipotembelea katika Hospitali ya Mnazi Mmoja mjini Unguja, leo Julai 19, 2012 kuwafariji wagonjwa waliolazwa hospitalini hapo baada ya kuokolewa katika ajali hiyo iliyotokea jana eneo la Kisiwa cha Chumbe. Kulia ni Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Muungano, Samia Suluhu Hassan. 

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akimsikiliza mmoja kati ya vijana walionusulika katika ajali ya Meli ya Skagit, Masembe Enos (32), mkazi wa jijini Mwanza aliyekuwa akisafiri na mkewe ambaye mpaka sasa hajapatikana.

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza na mgonjwa aliyenusulika katika ajali ya Meli ya Skagit, Hamisa Akida (45) mkazi wa Ununio mjini Bagamoyo, wakati alipotembelea katika Hospitali ya Mnazi Mmoja mjini Unguja, leo.

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza  mmoja kati ya vijana walionusulika katika ajali ya Meli ya Skagit, Stephano Lufyagila (22), mkazi wa Kiwalani jijini Dar es Salaam.

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza na vijana wawili, Hans Manoni (kulia) na Nsunga Joseph, waliokuwa wakisafiri na wenzao wawili ambao wamefariki katika ajali hiyo.

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akimsalimia Salome Abeid Mwambaga (33) mkazi wa jijini Arusha, mfanyakazi wa Kampuni ya Atomic Enegy Commissioner, aliyekuwa akisafiri kuelekea Pemba kikazi ambaye pia amepoteza vifaa vya kazi na Document zake zote muhimu katika ajali hiyo.

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Dkt. Ali Mohamed Shein, wakati alipofika Ikulu mjini Zanzibar leo kwa ajili ya kumpa pole kuhusu ajali ya Meli ya Skagit mali ya Kampuni ya seagull, iliyotokea jana eneo la Kisiwa cha Chumbe.

 Wananchi wakiwa wamepanga foleni kuelekea kutambua miili ya marehemu katika Viwanja vya Maisara leo.

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza na waandishi wa habari baada ya kujionea shughuli hizo katika viwanja vya Maisara mjini Unguja leo.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akijumjuika na wananchi katika moja ya familia iliyopotelewa na ndugu katika ajali hiyo, mjini Zanzibar leo mchana.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza na mgonjwa aliyenusulika katika ajali ya Meli ya Skagit, Hamisa Akida (45) mkazi wa Ununio mjini Bagamoyo. 

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Dkt. Ali Mohamed Shein, wakati alipofika Ikulu mjini Zanzibar leo Julai 19, 2012 kwa ajili ya kumpa pole kuhusu ajali ya Meli ya Skiget mali ya Kampuni ya seagull, iliyotokea jana eneo la Kisiwa cha Chumbe.
 
 

Orodha ya majina ya abiria wa MV Skagit itabandikwa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Dar es Salaam

19/07/2012
 
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam imebandika orodha ya majina ya wasafiri 340 waliokuwa katika meli ya Mv Skagit huku wananchi wakitakiwa kukuhakiki kama ndugu zao walikuwemo.

Aidha, Polisi jijini Dar es Salaam inamshikilia Meneja wa meli hiyo, Omar Hassan Mkamnhongt (50) mkazi wa Magomeni ambaye ni mmiliki wa Kampuni ya Seagul Transport Tawi la Dar es Salaam inayomiliki meli hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck amesema Polisi Kanda Maalumu inafanya uchunguzi wa ajali hiyo, wakishirikiana na wadau mbalimbali kusaidia utambuzi wa waliokufa, majeruhi wa Tanzania bara na wa Zanzibar pamoja na watalii kutoka nje.

Akizungumza na baadhi ya wanandugu waliofika ofisini kwake, Sadiki amesema, licha ya kubandika orodha hiyo, ofisi yake haina uhakika na idadi hiyo kwani huenda walikuwepo zaidi ya hao. Alisema orodha ya majina hayo itabandikwa katika ofisi yake na kwamba kila mwanandugu anayehitaji kufahamu zaidi anatakiwa kufika na kutambua majina hayo.

Alisema ofisi yake pia inajaribu kuzungumza na wamiliki wa meli au boti wasaidie wanandugu wanaotaka kwenda Zanzibar kutambua ndugu zao waliofikwa na mauti kwenye ajali hiyo, “Wapo wanandugu hapa ambao wana uwezo na wanataka kwenda Zanzibar ili kuwatambua ndugu zao, lakini wameshindwa kwenda kutokana na meli nyingine kusitisha safari hivyo hao tunakwenda nao bandarini sasa hivi (jana) ili kuwasaidia waweze kufanikisha safari yao,” alisema na kuongeza: “Kwa wale ambao hawawezi kwenda leo (jana) tutahakikisha tunafanya utaratibu ili kesho waweze kwenda kwa ajili ya kutambua maiti.

Kuhusu usalama wa meli hiyo, Sadiki alisema kwa mujibu wa taarifa za ukaguzi wa meli hiyo, inaonesha kwamba ilikaguliwa Agosti 24 mwaka jana na kwamba ilikuwa inamalizika muda wake Agosti 23, mwaka huu, “Si kweli kwamba meli ilikuwa haijafanyiwa uchunguzi… polisi wanafuatilia zaidi… na kuanzia leo (jana) tunatengeneza fomu maalumu yenye jina la aliyepotea na anayetaka kwenda Zanzibar kutambua maiti ambapo ataandikisha jina lake kwa Edward Mbanga aliyeko katika ofisi za Mkuu wa Mkoa,” alisema.

Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema juzi walituma kundi kubwa la watu kwa ajili ya kusaidia shughuli ya kuokoa.

Kova aliwataka ndugu na jamaa wa watu wanaohofiwa kufa katika meli hiyo, waorodheshe majina ya ndugu zao, nguo walizokuwa wamevalia ili kikosi chake kwa kushirikiana na Mamlaka ya Usafiri wa Majini na Nchikavu (Sumatra) walioko eneo la ajali, wasaidie kuwatambua.
  

"Kuna watu 11 wakiwamo waandishi 2 wa habari, nitawatwanga kweupe" - Membe

19/07/2012
 
Juzi alipozungumza katika kipindi cha dakika 45 kinachorushwa na Kituo cha Televisheni cha ITV na kuongozwa na Mtangazaji wa ITV, Selaman Semeyu, Waziri wa Mambo ya Nje ya Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe alizungumzia pamoja na mambo mengine, fedha za mkopo, Dola za Marekani milioni 20 zilizokuwa zimetolewa na Serikali ya Libya enzi za utawala wa aliyekuwa rais wa nchi hiyo, Hayati Muamar Gaddafi.

Pia aligusia upotevu wa Sh bilioni tatu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Akizungumzia fedha hizo, Membe alisema baada ya Serikali ya Libya kuikopesha Serikali ya Tanzania kiasi hicho cha fedha, baadaye Serikali za nchi hizo mbili zilikutana na kukubaliana fedha hizo zikopeshwe kwa kampuni yoyote itakayozihitaji.

“Baadaye Serikali ya Libya na Tanzania zilikutana na kukubaliana fedha hizo zikopeshwe kwa kampuni yoyote itakayotaka kukopa izikope na makubaliano haya yako kwenye maandishi. Baadaye ikaja kampuni moja ya Meize kwa ajili ya kujenga kiwanda cha saruji kule Lindi na wakati wa kampeni tukawaahidi wananchi wa Lindi kwamba kiwanda hicho kitajengwa. Wakati tunaahidi hivyo, kumbe Kampuni ya Mohamed Enterprises ilikuwa inashirikiana na ofisa mmoja wa ubalozi wa Libya apate fedha hizo na hapo ukawa ugomvi.

“Pamoja na hayo, mimi nilisimamia kuhakikisha kiwanda hicho cha saruji kinajengwa Lindi kama sehemu ya kumbukumbu yangu. Lakini baadaye wananume wakabadilisha lugha, wakasema nimewapa marafiki zangu, jamani fedha hizi ni makubalino ya nchi mbili na mimi ni ‘share holder’.

“Sasa nakwambia fedha hizi ziko TIB, nendeni kwa meneja wa TIB mumuulize, huu ujinga gani huu unaozungumzwa, kwanza hata hizo Dola milioni 20 hazitoshi kujenga kiwanda bali zinatakiwa Dola milioni 60.

“Sasa nataka niwaambie wananchi wa Lindi kwamba kiwanda cha saruji kitajengwa Lindi, hivi vituko vinavyotokea nitavigonga vyote na ipo siku nitawaanika wote, lazima watu hao wajue kwamba ukikaa juu ya nyoka, ipo siku atakugonga tu. Hili nawaachia Watanzania waamue lakini kuna watu 11 wakiwamo waandishi wawili wa habari, nitawatwanga kweupe, nyie suala la urais 2015 subirini tu nitawaanika peupe bungeni tena kwa majina,” alisema Waziri Membe.

Suala la urais 2015

Alipoulizwa kama atagombea urais mwaka 2015, alishindwa kuweka wazi msimamo wake kwa kile alichosema kuwa hajaoteshwa juu ya nafasi hiyo.

“Ole wao nioteshwe, ipo siku nitaoteshwa, najua nchi hii ina watu wanaoivuruga na hawataki kuona mafanikio, ukisema unataka kujivua gamba utaona wana uwezo wa kuchonga uongo, hao wanatumia vyombo vya habari kuchonga uongo. “Kwa mfano, unawakaribisha vijana kama wa Chadema nyumbani kwako unawapa chakula baadaye wanageuza mambo, we waache tu.

“Siku moja nitawatoa kwenye magazeti kila mmoja dozi yake, nitakuja kuwatandika kila mmoja na kinachoniudhi ni kwamba hao watu wako ‘smart’ wana fedha na wanataka kutawala hata kama hawana madaraka. Ukiona mtu anaanza kudharau wakati hana madaraka, ujue hapo kuna tatizo. “Jambo jingine ni kwamba ukianza kuona katika jamii kila tatizo inalaumiwa Serikali, ujue kuna tatizo, ujue hapa kazi ipo.

Uchaguzi ndani ya CCM

Kuhusu uchaguzi unaoendelea ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), alisema chama hicho kina nafasi ya kujiimarisha kupitia uchaguzi huo. Alisema ana hamu ya kufika mwaka 2015 ashuhudie uchaguzi mkuu utakavyokuwa.

“Nina hamu ya kufika mwaka 2015 nione akina nani watarudi maana kuna wabunge wengine ni mahodari wa kuzungumza bungeni lakini majimboni hawaendi. “Utakuta mbunge mwingine anasema haungi mkono bajeti, lakini baada ya siku mbili anamuomba Waziri aliyepinga bajeti yake kwamba naomba fedha za kupeleka jimboni kwangu. “Upinzani siyo kukataa bajeti, huwezi kukataa bajeti yangu halafu kesho unakuja kuniomba fedha upeleke jimboni kwako,” alisema.

Alitaka Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni naye awe anaulizwa maswali ya papo kwa papo kupima uwezo wake katika utendaji.

Maoni ya wabunge

Wakizungumza juu ya kauli za waziri huyo, baadhi ya wabunge wameonyesha kutoridhishwa kutokana na nafasi aliyonayo katika Serikali.

Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina (CCM), alisema kitendo cha Membe kusema kuna watu 11 wanaiyumbisha Serikali, hakitakiwi kufumbiwa macho kwa kuwa kinagusa mamilioni ya Watanzania, “Huyu Membe aache maneno, hivi majuzi alisema kuna watu anawafahamu wanahusika na mauzo ya rada, sasa anakuja na suala jingine la watu 11 wanaoyumbisha nchi. “Kama kweli anawajua kwa nini asiwataje, yaani wananchi wanataabika halafu yeye anatwambia atawataja, mimi simuelewi, mwambieni awataje,” alisema Mpina.

Mbunge wa Nyamagana, Ezekiah Wenje (CHADEMA), alisema Membe anatafuta umaarufu wa siasa kwa kuwa ana kitu anachokitaka, “Huyu tumemzoea, alisema hivi karibuni kwamba anawajua wahusika wa rushwa ya rada na hadi sasa hawajawataja, sasa unafikiri anataka nini. “Kama kweli hao watu wapo kwa nini asiwataje, atutajie majina, lakini kama anadhani kuna watu kama akina Lowassa wanataka kumkwamisha asigombee urais mwaka 2015, anajidanganya kwa sababu yeye hawezi kupambana na Lowassa, huyo ni mtu mdogo kwa Lowassa,” alisema Wenje.

Naye Mbunge wa Kinondoni, Idd Azzan (CCM), alionyesha kutoridhishwa na kauli ya Membe na kusema kuwa hakumuelewa baada ya kutotaja majina ya watu hao 11.

“Mimi nilimuona akizingumza na nilipomsikia hivyo, nikashindwa kumuelewa kwa sababu kama alichokuwa akikisema hakiendani na madaraka yake. “Sasa kama kweli anawajua watu hao 11 kwa nini asiwataje, atutajie kuwafanya wananchi waendelee kuiamini Serikali yao,” alisema Azzan.

Rais mmoja mstaafu wa Zanzibar atajwa kuhusika na usajili wa Meli za Iran

 
Wakati uchunguzi wa kimataifa ungali ukiendelea, gazeti la Raia Mwema limethibitishiwa kuwa Rais mstaafu aliyepata kuongoza Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) na mmoja wa kigogo wa juu wa sasa wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa, wanahusika.

Mtandao huo wa kiongozi huyo mstaafu ambaye anazo ndoto za kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na mwenzake ndani ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa, wamefanya mpango huo na aliyepata kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM), ambaye pia amepata kuwa mbunge wa moja ya majimbo ya uchaguzi mkoani Tabora.

Kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari, tayari vyombo vya kimataifa vinaelekea kukamilisha uchunguzi wake na kwamba, majina ya wahusika hao yatawasilishwa serikalini kwa hatua zaidi.

Kwa ushirikiano maalumu, viongozi hao wanadaiwa kufanikisha meli za Iran kusajiliwa na kisha kupeperusha bendera ya Tanzania kwa lengo la kukwepa vikwazo vya kimataifa vilivyoweka kupitia Umoja wa Mataifa (UN).

Vigogo hao wanadaiwa kufanikisha mpango wao kupitia kwa kampuni ya Philtex ya Dubai, inayodaiwa kusajili meli za mafuta za Iran ili kupeperusha bendera ya Tanzania kwa lengo la kukwepa vikwazo vya kiuchumi iliyowekewa nchi ya Iran.

Katika toleo lake namba 248, gazeti hili liliripoti kuwapo kwa taarifa kutoka kwa baadhi ya maofisa wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa zikibainisha kuwa, baadhi ya viongozi Zanzibar wamekuwa na maslahi katika masuala ya usajili wa meli hizo za kimataifa jijini Dubai.

Katika habari hiyo kwenye gazeti hili, mwandishi wetu alinukuu moja ya chanzo chetu cha habari akisema; “Unajua kuna hali ya kuzidiana ujanja, awali huku Zanzibar walikataa SUMATRA (Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Maji na Nchi Kavu) kufanya shughuli zake na wakaunda Wakala wa Meli Zanzibar (ZMA) lakini wakala huyu akatoa zabuni ya kusajili meli kwa kampuni iliyoko Dubai (Philtex),”

“Baadhi ya viongozi hapa Zanzibar hawakujua ujanja uliopangwa na wenzao, ujanja wa kuikataa SUMATRA Zanzibar na kuanzisha ZMA lakini pia ujanja wa kutoa zabuni kwa kampuni ya Philtex ya Dubai. Sasa hivi ndiyo wanashituka kwamba wapo wenzao wanaodaiwa kuhusishwa na kampuni hiyo,” kilieleza chanzo chetu cha habari kutoka Serikali ya Zanzibar.

Ya TANESCO: Akaunti ya kigogo ya Bil. 1/- yazuiwa; Hujuma; Wabunge wanahusishwa


 
SIKU chache baada ya kusimamishwa kazi kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme (TANESCO), William Mhando na wenzake: Robert Shemhilu, Lusekelo Kassanga na Haruna Mattambo, akaunti ya mmoja wa vigogo wa shirika hilo ngazi ya menejimenti iliyoko katika moja ya benki nchini imezuiwa na vyombo vya dola nchini, Raia Mwema, limeelezwa.

Akaunti ya kigogo huyo (jina la benki na la mwenye akaunti yanahifadhiwa ili kutoharibu uchunguzi unaoendelea) imekutwa na fedha zaidi ya shilingi bilioni moja na sasa inadaiwa kuzuiwa kwa baraka za mamlaka za juu.

Vyanzo kadhaa vya habari vimeeleza ya kuwa kigogo huyo amekutwa na mabilioni hayo ya fedha huku chanzo cha mapato hayo yasiyolingana na kipato chake kama mtumishi wa umma kikiwa ni utata.

Hata hivyo, wakati uchunguzi huo wa awali unaofanywa na vyombo vya dola nchini ukiwa unaendelea, kwa upande mwingine kumebainika kuwapo na kampeni kali za kuuokoa uongozi wa TANESCO unaochunguzwa kwa sasa, juhudi ambazo zimekuwa zikihusisha hata Kamati za Bunge.

Kamati za Bunge ambazo baadhi ya wajumbe wake wanahusishwa katika ‘kuokoa’ jahazi la uongozi wa TANESCO uliosimamishwa ni pamoja na Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma.

Baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo sasa wanatajwa kuanza kumwandama Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi pamoja na Waziri Profesa Sospeter Muhongo na Naibu wake, George Simbachawene, wanaotajwa kuwa na msimamo mkali dhidi ya kile kinachodaiwa kuwa ni uzembe na ubadhirifu ndani ya TANESCO.

Mgawo feki wa umeme
Hujuma kwa mtambo wa Kinyerezi
Wabunge watajwa

Tume ya Katiba yatoa taarifa ya kusitisha mikutano ya kukusanya maoni kwa siku tatu


 
Alhamisi, Julai 19, 2012

Tume ya Mabadiliko ya Katiba imepokea kwa masikitiko makubwa Taarifa ya ajali ya Meli ya MV SKAGIT iliyotokea jana, Jumatano, tarehe 18,  Julai  2012 katika eneo la Chumbe, Zanzibar.

Kutokana na msiba huu mkubwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba inatoa Taarifa kwa Wananchi kuwa imesitisha Mikutano ya kukusanya Maoni ya Wananchi kuhusu Katiba Mpya iliyokuwa inaendelea katika Mkoa wa Kusini Pemba. Mikutano iliyositishwa ni ile iliyopangwa kufanyika kuanzia leo, Alhamisi, Julai 19, 2012 hadi Jumamosi, Julai 21, 2012 katika maeneo ya Wawi, Vitongoji, Chanjamjawiri, Pujini, Gombani na Wara.

Zoezi la kukusanya Maoni litaendelea kuanzia  Jumapili tarehe 22, Julai, 2012.  Ratiba ya Mikutano katika maeneo yaliyositishwa itatolewa baadaye.

Tume ya Mabadilikio ya Katiba inapenda kuwafahamisha wananchi kuwa mabadiliko haya hayahusu mikutano ya kukusanya maoni inayoendelea kufanyika katika mikoa sita (6) ya Tanzania Bara ambayo ni Pwani, Tanga, Dodoma, Shinyanga, Kagera na Manyara.  Tume inawaomba wananchi wa Mikoa hii kujitokeza kwa wingi na kutoa maoni yao.

Mwisho, Tume ya Mabadiliko ya Katiba inatoa pole kwa wafiwa, majeruhi na wote walioguswa na ajali hii na tunamuomba Mwenye Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi na majeruhi wote wapone kwa haraka.

Imetolewa na:
Tume ya Mabadiliko ya Katiba,
S.L.P. 1681,
DAR ES SALAAM,
Simu: 2137833,
Simu ya Mkononi: 0757 500800