KATIBA YA NCHI SI MALI YA
WANA CCM ASEMA HASSAN NASSOR MOYO MUASISI WA MAPINDUZI NA MUUNGANO WA TANZANIA, ATAKA
CCM ISIHODHI MJADALA WA KATIBA.
01/08/2012
Mwanasiasa
Mkongwe Hassan Nassor Moyo akizungumza na Waandishi wa Habari
mbalimbali kuhusiana na Mambo ya Muungano hapo katika Ukumbi wa Hoteli
ya Rumaisa Bwawani Zanzibar (picha: ZanzibarYetu.wordpress.com)
Na Abdallah Vuai
Katiba ya nchi sio mali ya
Chama cha siasa, ingawaje baada ya Muungano wa Tanganyika
na Zanzibar vyama vingi vya siasa vilifutwa na
kutangazwa kuwepo kwa vyama viwili tu yaani ASP kwa Zanzibar
na TANU kwa Tanganyika,
hivyo kufanya katiba kuwa mali
ya vyama hivyo.
Ilivyokuwa katiba katika Taifa lolote la kidemokrasia, lenye kuheshimu misingi
ya utu ni mali
ya wananchi na hivyo ni wananchi pekee ndiyo wenye haki ya kubadili katiba ya
taifa lao.
Aidha, katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni ya Watanzania wote na
kamwe si ya chama tawala cha CCM, makada wake au makamanda wa vita vya ufisadi,
hivyo si haki suala la mabadiliko ya katiba ya nchi yakafanywa ni maagizo
elekezi ya kufuatwa na wananchi na zaidi wanachama wa CCM.
Kwa sasa CCM haina uhalali sio tu wa kuhodhi katiba ya nchi bali hata kutoa
agizo kwa umma kwamba wafuate mtazamo wake katika kutoa maoni juu ya katiba
mpya. Natambua kuwepo kwa msimamo wa CCM kuhusu wanachama wake kuwataka wakatoe
maoni katika Tume ya Jaji Warioba wasema wanataka Serikali mbili!
Hapa leo ndipo hoja yangu itakapojikita,lakini zaidi nitautizama msimamo huo wa
CCM kwa upande wa pili wa shilingi kwamba ikiwa kuna wanachama wasiokubaliana
na maoni hayo ya ‘kupewa’ nini tafsiri yake? Lakini pia katika nchi huru yenye
kufuata misingi ya haki za binadamu kwa kuzingatia katiba ya nchi, haipendezi
kuwalazimisha watu kuacha maoni yao
kufuata ya Chama au kikundi fulani.
Msimamo wa CCM kuwashurutisha wanachama wake kwenda kusema wanataka Serikali
mbili umewanyang’nya haki ya kimsingi ya uhuru wa kufikiri,lakini pia tunaweza
kupata katiba mbovu yenye mawazo yanayolingana na hii naweza kuitafsiri kuwa
zile nguvu za
watawaliwa kuwadhibiti watawala
zimeondolewa na kuwa kinyume chake watawala kuwadhibiti watawaliwa.
Watu wafahamu kuwa kama kuna nchi ikaanza
kutoa maoni na mapendekezo yake kwa wananchi ili wachangie kwa lengo la
kufanyia mabadiliko katiba ya nchi, tambua kuwa katiba inayotaka kutungwa au
kurekebishwa ni ya watawala.
Katika hili lazima wananchi na hasa Wazanzibari waelewe kwamba katiba ya nchi
inapaswa kuwa ni mali yao na tena inayo mahusiano ya moja kwa moja na maisha yao ya kila siku na kwa muktadha
huo ni lazima pia mabadiliko yoyote yaanze kutoka kwao.
Akina Nape Nnauye mnaposema mwana CCM atakayekwenda kutoa maoni tofauti na
yaliyobatizwa na NEC ya Chama chenu ni kuviza demokrasia na kuwafanya wanachama
wenu uwezo wao wa kufikiri mdogo jambo ambalo mimi siliamini hata kwa mtutu wa
bunduki.
Dola ya Tanzania inaongozwa
na CCM ni jambo la kustajabisha Chama hicho kinapingana na uamuzi wa Serikali
yake katika suala zima la katiba mpya, kwamba Rais Jakaya Kikwete ameunda Tume
ya Mabadiliko ya Katiba ili kupata maoni ya wananchi kuhusu jambo hilo, kama CCM haikuwa
ikitaka mawazo tofauti wangeiambia Serikali isiunde Tume.
CCM kuwafunga midomo wanachama wake ni sawa na kuwa na kiungo katika mwili
kilichopooza ambacho hakiwezi kufanya jambo lolote kimezidiwa hata na mwana
sesele anayetiwa betrii akacheza cheza.
Tunashukuru Mungu kuwa katika Mkoa wa Kusini Unguja si wanachama wa CCM wala wa
vyama vyengine waliofuata maagizo elekezi ya vyama vyao, bali wametoa mitazamo yao na ndio maana kwenye
ngome ya CCM Kusini Unguja maoni ya kutaka mabadiliko katika mfumo wa muundo wa
Muungano yameshika kasi.
Kwa maana nyengine wameyapuuza maagizo elekezi ya Chama chao, hivyo CCM na
viongozi wake wanapaswa kujithamini upya maana hali ndio hiyo ule wakati wa
‘zidumu fikra za Mwenyekiti’ umeshapita, hakuna mawazo ya kushikiwa.
Mara nyingi CCM haijifunzi kutokana na makosa yake, kama wangekuwa wanajifunza
matokeo ya ripoti ya Jaji Nyalali na Jaji Robert Kisanga wasingekuja na maagizo
yasiyotekelezeka kwa wanachama wao maana kwa wakati ule asilimia kubwa walitaka
mabadiliko katika Muungano, hawakuchangia maoni kama
walivyotakiwa na Chama chao.
Sote tunafahamu matokeo ya ripoti ya Jaji Kisanga, Chama tawala na Rais wake
kwa wakati huo Benjamin Mkapa walikuwa wakali na kwa sehemu kubwa walichukizwa
na taarifa hiyo kwa sababu ilidhihirisha kwamba si wananchi wala Kamati
inayokubaliana na matakwa ya Watawala.
Tunaelezwa kwamba ni wananchi laki sita tu ndio
waliochangia maoni na katika hao wapo pia waliopinga moja kwa moja maoni ya
serikali, na kubakisha idadi ndogo tu ya wananchi wasiozidi laki nne
waliokubaliana na maoni ya Serikali.
Wengi hawakwenda kutoa maoni yao na hii inaweza
kusababishwa na mambo mengi,lakini kubwa ni kwamba wananchi hawa ni watu wazima
wenye akili timamu hawapendi maoni ya kupewa mkononi, kila mtu yuko huru na hilo limethibitishwa na
kupewa nguvu kwenye katiba yetu.
Hatutaki kuamini kwamba haki na demokrasia ni maneno tu yanayotumiwa na Chama
tawala ili kuwalaza usingizi mnono wananchi huku wakinyimwa haki yao ya msingi ya
kushiriki kutoa maoni wanayoyaona yanafaa.
Wazanzibari wakati umefika sasa tukaachana na ushabiki wa vyama vya siasa
tukaendelea na juhudi zetu kudai mabadiliko katika mfumo wa muundo wa Muungano
na bila shaka tuungane kufikiria kuhusu mustakbali na hatima ya nchi yetu Zanzibar vyenginevyo, kwa
‘kuiendekeza’CCM itatufikisha ging’ingi.
Hali ya kiuchumi tuliyonayo Zanzibar kwa miaka
48 ni matokeo ya mfumo mbovu wa muundo wa Muungano, sera zake za kiuchumi
haziisaidia Zanzibar
kuwapeleka mbele katika kuwa na uchumi endelevu na imara, tutaendelea kusambaza
bakuli kwa wajomba mwisho watatuchoka.
Kama unalo wazo ambalo unadhani linaweza likaleta manufaa usikae kimya kwa
kuhofia tamko la kina Nape, Vyama vya siasa ni vya kupita tu,lakini Zanzibar itaendeela
kuwepo, tujiulize viko wapi leo vyama vya siasa kabla ya Mapinduzi?
CCM wasifikiri Wazanzibari wamelala usingizi fofofo, ikiwa wataamini hivyo basi
wakae wakijuwa kuwa kioo kimewacheza kizazi cha leo cha Zanzibar sio kile cha mwaka 1964 na kwa
kuthibitisha haya tazama maoni yaliyotolewa Mkoa wa Kusini Unguja kuhusu katiba
mpya.
Mlalahoi mwenzangu fahamu kwamba unapowasikia viongozi wa CCM, wakihubiri
kwamba wametoa mamauzi yale kwa sababu ndivyo wananchi wanavyotaka, kaa ukijuwa
wananchi wanaokusudiwa hapo ni vigogo wenziwao, wewe mlalahoi unaeishi Mwakaje,
Mikunguni, Fuoni, Darajabovu, Chumbuni huna chako, wewe utapewa wali na pilau,
kanga na kikoi na kisha utupwe kwenye mavumbi mpaka baada ya miaka mitano tena
ndio ukumbukwe kuja kupewa tena pilau, kanga na kikoi.
Vyama vya siasa kuanza kuwatisha wanachama wake kuwafukuza uanachama ni sawa
kuwafanya watumwa ndani ya nchi yao,
maana watakuwa si huru kusema yale wanayoyataka, wakitoa maoni tofauti ambayo
hayawapendezi Muhafidhina wataanza kutumia rungu la Chama kutisha wanachama.
Kwa tamko la CCM tafsiri yake ni kwamba watu hawana uhuru wala haki ya kutofautiana mawazo. Yeyote anayetofautiana na
tamko hilo anahesabiwa kama
muasi,mchochezi, msaliti.
Ni jambo la kusikitisha kuona Tanzania
baada ya miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika
na miaka 48 ya Mapinduzi ya Zanzibar watu
wanakosa uhuru ndani ya nchi huru basi hawezi kuendelea hata kama nchi hiyo
ingerundikiwa utajiri wote wa dunia, kama leo
mtu anafundishwa au anashurutishwa kutoa maoni yasiyoyake na asiyeyaamini hili
ni tatizo kubwa katika demokrasia yetu.
Tukumbuke kuwa nchi nyingi zilizopiga maendeleo watu wake walikuwa na uhuru, watu
wasio huru hawawezi kusonga mbele kimaendeleo kila siku tukariri kama kasuku maoni ya watu fulani na ndio maana mipango
mingi ya maendeleo haitekelezeki kwa sababu haikupangwa na watu wenyewe,
imepangwa na wakubwa Serikalini.
Kwa sasa Wazanzibari tuna vipaumbele vyetu katika katiba na zaidi kuliko yote
suala zima la Muungano watu wanataka mabadiliko katika mfumo wa muundo wake,
wameuchoka muundo wa sasa ambao hauwaletei faida za kiuchumi.
Hivyo basi, suala la kutoa maoni kuhusu katiba mpya kutekwa nyara na tamko la
CCM ni kudhihirisha kuwa madai ya wananchi kwamba CCM, wanaelekea kuwa na nia
ya kutokuheshimu matakwa ya wananchi katika kuilea na hatimae kuikuza
demokrasia ya kweli Tanzania.
Wengi tunaamini kuwa katiba ndio nguzo ya Taifa na pia ndio sheria kuu ya nchi,
kwa sababu hiyo, kigezo cha kwanza cha kuthibitisha kama
kweli nchi ina muelekeo wa kidemokrasia ni kuonekana kwa misingi ya demokrasia
katika mchakato wa utoaji maoni katika Tume ya Jaji Warioba.
CCM inaelekea kutaka kukumbatia utawala wa kiimla, kwa kuwalazimisha watu
kusema wanayotaka wao. Watu wa Tanganyika
wanayao katika mabadiliko ya katiba, watu wa Zanzibar
pia wana mambo yao
ambayo jambo la kwanza kabisa ni Muungano.
Je, wanachama wa CCM watabakia kama watu wa
kusadiki kila kitu au watafuata wosia wa Mwenyekiti wao, Jakaya Kikwete
aliposema akili za kuambiwa changanya na zako.
Baadhi
ya Waandishi wa Habari mbalimbali waliohudhuria Katika Mkutano wa
Mwanasisa Mkongwe Hassan Nassor Moyo akizungumzia mambo ya Muungano hapo
katika Ukumbi wa Hoteli ya Rumaisa Bwawani Zanzibar. (picha:
ZanzibarYetu.wordpress.com)
Mwisho kabisa mwa hotuba (kwa
maandishi) kuna pleya yenye audio ya maswali ya Wanahabari na majibu ya Rais.
HOTUBA YA MHE. DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE,
RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,
KWA WANANCHI, TAREHE 31 JULAI, 2012
Ndugu Wananchi;
Naomba
nianze kwa kuomba radhi kwa kutoa hotuba ya mwisho wa mwezi wa saba,
leo tarehe 01 Agosti, 2012 badala ya jana tarehe 31 Julai, 2012. Hii ni
kwa sababu ya msiba uliotukuta katika familia na mimi kwenda Lindi
kushiriki maziko ya marehemu wetu. Tofauti na miezi iliyopita leo,
pamoja na hotuba ya kawaida ya mwisho wa mwezi nimetoa fursa kwa
Wahariri wa vyombo vya habari nchini kuniuliza maswali nami kujibu. Kwa
upande wangu nina mambo matatu ambayo nitayazungumzia leo.
Ajali ya Kuzama kwa Meli ya MV SKAGIT
Ndugu Wananchi;
Jambo la kwanza ni ajali ya Meli ya MV SKAGIT iliyotokea tarehe 18 Julai, 2012. Meli hiyo ilikuwa na watu 290, wakiwemo mabaharia 9,abiria watu wazima 250 na watoto 31. Juhudi
za uokoaji zilianza mara baada ya taarifa ya kuzama kwa meli hiyo
kupatikana. Maofisa na askari wa JWTZ, Polisi na KMKM walishiriki
pamoja na meli na watu binafsi katika uokoaji. Waokoaji walifanikiwa
kuwapata ndugu zetu146 wakiwa hai na maiti 126 hadi
tarehe 27 Julai, 2012. Kwa maana hiyo basi, watu 18 hawajulikani
walipo na inahofiwa kuwa nao pia hawako hai. Huenda wamezama pamoja na
meli au walizama baharini lakini miili yao haikuweza kupatikana.
Ndugu Wananchi;
Napenda
kutumia nafasi hii kurudia kutoa mkono wa rambirambi na pole nyingi kwa
wale wote waliopoteza ndugu, jamaa na marafiki katika ajali
ile. Nampongeza sana Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein na viongozi wenzake wa
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kwa kazi kubwa na nzuri waliofanya
kuongoza juhudi za uokoaji pamoja na huduma walizotoa kwa waliokolewa,
waliojeruhiwa na waliofariki. Kwa wale ambao walikuwa wenyeji wa Unguja
na Pemba, SMZ ilitoa sanda na usafirishaji wa maiti mpaka makwao kwa
mazishi. Kwa wale wasiokuwa na ndugu Serikali ilibeba jukumu la
kuwazika kule Kama, Kusini Unguja.
Natoa pongezi za pekee kwa
wale wote walioshiriki katika uokoaji kwani juhudi zao ziliwezesha ndugu
zetu wengi kusalimika na maiti nyingi kupatikana.
Ndugu Wananchi;
Kutokea
kwa ajali ile kumetonesha jeraha la huzuni, majonzi na mashaka makubwa
yaliyolipata taifa letu miezi 11 iliyopita kufuatia ajali ya kuzama kwa
meli ya MV Spice Islander. Katika mkutano maalum wa Baraza la Usalama
wa Taifa niliouitisha tarehe 20 Julai, 2012 kuzungumzia ajali ya MV
SKAGIT tulifanya mapitio ya utekelezaji wa maagizo yetu ya mkutano wa
tarehe 11 Septemba, 2011 kufuatia ajali ya MV Spice Islander. Kwa
ujumla tumeridhika kuwa utekelezaji umekuwa mzuri kwa upande wa mamlaka
zinazohusika na usafirishaji majini yaani SUMATRA, Zanzibar Maritime
Authority na mamlaka za Bandari za nchi zetu mbili. Ushirikiano baina
ya mamlaka hizo sasa ni mzuri kwa mambo yote muhimu ambayo Baraza
liliagiza wafanye hivyo. Pamoja na hayo Baraza limetaka ushirikiano
huo uzidishwe na kuimarishwa.
Kwa mfano, Baraza limefurahishwa na
kupongeza kitendo cha mamlaka hizo kutumia Dar es Salaam Maritime
Institute kwa ushauri kuhusu ubora wa meli na huduma za usafirishaji
majini. Baraza limeagiza vyombo hivyo viwe na hadidu za rejea
zinazofanana kwa vigezo vya ubora ili nchi yetu iwe na viwango
vinavyofanana vya ubora wa meli na huduma za usafirishaji baharini kwa
pande zetu mbili za Muungano. Bahari ni moja na vyombo vinahudumia watu
wale wale, kuwa na vigezo tofauti vya ubora wa meli na viwango vya
huduma ni jambo lisilostahili kuwepo tena, ni la hatari. Baraza pia
limeagiza pawepo na ukomo wa umri wa meli zilizokwishatumika
zinazoruhusiwa kutumika hapa nchini.
Aidha, Baraza limerudia
kuagiza pawepo na usimamizi makini zaidi kuhusu upakiaji wa mizigo na
abiria. Mamlaka husika, yaani SUMATRA, ZMA na maofisa wa
bandari wahakikishe kuwa uwezo wa meli uliohakikiwa na kutambuliwa
unaheshimiwa ipasavyo. Pia, meli zikaguliwe mara kwa mara na vigezo
vifanane.
Ndugu Wananchi;
Pamoja
na hayo, Baraza la Usalama wa Taifa limeona kuwa wakati umefika kwa
Serikali yetu kuwa na Coast Guards, yaani kikosi maalum cha uokoaji na
usalama majini. Aidha, Baraza limetaka hatua za makusudi zichukuliwe
kuimarisha KMKM na Police Marines. Mwisho, Baraza lilipongeza uamuzi wa
SMZ wa kuunda Tume ya kuchunguza ajali ile kama ilivyofanya wakati wa
ajali ya MV Spice Islander.
Utafutaji na Uchimbaji Gesi Nchini
Ndugu Wananchi,
Jambo
la pili ninalopenda kulizungumzia leo ni kuhusu maendeleo ya sekta ya
gesi asili nchini. Juhudi za kutafuta mafuta nchini zilianza mwaka 1952
na mwaka 1954 wakati kampuni ya BP ilichimba kisima cha kwanza kule
Mafia. Bahati mbaya kisima hicho hakikuzaa matunda yaliyotarajiwa na
juhudi za utafutaji mafuta zikafifia kabisa mwanzoni mwa miaka ya
1960. Miaka kumi baadae, juhudi hizo zilianza upya na kuendelea kwa
kiwango na kasi za namna mbalimbali hadi sasa. Katika miaka ya hivi
karibuni juhudi zimekuwa kubwa na kuhusisha makampuni kadhaa ya
kimataifa yakiwemo makubwa na madogo.
Ndugu Wananchi;
Tangu mwaka 1954, mpaka sasa visima 61 vimechimbwa, kati ya hivyo, gesi asili imegunduliwa katika visima 22, visima 14 vya nchi kavu na maeneo ya maji mafupi na visima 8vya
bahari ya kina kirefu. Hatujabahatika kupata mafuta lakini
tumefanikiwa kupata gesi asili katika maeneo kadhaa baharini na nchi
kavu katika mikoa ya Mtwara, Lindi na Pwani.
Kwa mujibu wa
taarifa zilizopo kutokana na visima vilivyochimbwa mpaka sasa, akiba ya
gesi asili iliyopo nchini inakadiriwa kuwa kati ya futi za ujazo trilioni 25.4 – 28.9. Yapo
matumaini makubwa ya gesi nyingi zaidi kugundulika katika miaka
michache ijayo. Hii ni kutokana na ukweli kwamba shughuli za utafutaji
mafuta na hasa gesi baharini zilizoanza mwaka 2004 kukiwa na kampuni
moja sasa zipo 18. Baada ya ugunduzi wa kwanza
wa gesi mwaka 2010, shughuli za utafutaji sasa zimepamba moto na
zimekuwa na mafanikio. Naamini gesi nyingi zaidi itaendelea kupatikana.
Fursa za Maendeleo
Ndugu Wananchi;
Kwa
kiasi cha gesi asili kilichokwishagunduliwa na kwa matumaini yaliyopo
ya gesi zaidi kupatikana kunaifanya Tanzania kuwa moja ya nchi za
kutumainiwa duniani kwa upatikanaji wa gesi asili miaka michache
ijayo. Hali hiyo inaipa nchi yetu fursa kubwa ya kuweza kujiletea
maendeleo makubwa ya kiuchumi na kijamii muda si mrefu kutoka sasa.
Gesi
asili ni rasilimali inayoweza kutumika kuzalisha mbolea na hivyo
kusaidia katika kuendeleza kilimo nchini kwa kurahisisha upatikanaji
wake na kuwa ya bei nafuu. Gesi asili inaweza kutumika kuzalisha umeme
na hivyo kuiwezesha nchi kupata umeme wa kutosha na kuwepo ziada ya
kuuza nje. Hivi sasa, katika gridi ya taifa megawati 350za umeme zinatokana na gesi asili na hata lengo letu la kuzalisha megawati 3,500 ifikapo
maka 2015 tunategemea zaidi gesi asili kuwezesha hilo kutimia. Ujenzi
wa bomba la gesi kutoka Mtwara kuja Dar es Salaam una shabaha hiyo.
Ndugu Wananchi;
Vile
vile, gesi asili inaweza kutumika kutoa nishati viwandani badala ya
kutumia mafuta na hivyo kupunguza gharama za uzalishaji. Watu majumbani
wanaweza kutumia gesi asili kupikia hivyo kupunguza matumizi ya umeme,
mafuta, mkaa na kuni. Inapunguza gharama za maisha na kusaidia
kuhifadhi mazingira kwa kupunguza ukataji wa miti. Ni kutokana na
kutambua ukweli huo ndiyo maana TPDC inatekeleza mradi wa kutengeneza
gridi ya mabomba ya kusambaza gesi majumbani katika jiji la Dar es
Salaam.
Jambo lingine muhimu kuhusu rasilimali hii ni kwamba tukiuza
nje gesi nchi yetu itapata mapato mengi tena ya fedha za kigeni. Kwa
vile gesi ni nyingi mapato ya Serikali yataongezeka sana, hivyo
kuijengea uwezo wa kutimiza majukumu yake vizuri zaidi. Kama matumizi
yatakuwa mazuri, gesi asili itakuwa kichocheo kikubwa cha kukuza uchumi
wa nchi. Maendeleo ya haraka yatapatikana na hivyo kusaidia kuwaondoa
wananchi wengi kutoka katika lindi la umaskini tulionao sasa.
Changamoto Muhimu
Ndugu Wananchi;
Pamoja
na ukweli kwamba kuwa na gesi asili nyingi kunaipa nchi yetu fursa
kubwa ya kujiletea maendeleo, zipo pia changamoto zake. Hatuna budi
kuzitambua na kuzitafutia ufumbuzi ili gesi iweze kunufaisha ipasavyo
nchi yetu na watu wake. Changamoto zipo nyingi lakini kubwa zipo za
namna tatu.
Changamoto ya kwanza ni ile ya kujenga uwezo wetu
wenyewe wa kudhibiti shughuli zinazofanywa na makampuni ya mafuta ili
tuhakikishe kuwa tunapata malipo yanayostahili. Inatulazimu tuwe na
wataalamu wetu wazalendo wa fani za taaluma zihusuzo gesi kama vile
uhandisi, kemia, jiofizikia, uhasibu, ukaguzi na sheria. Tusipojenga
uwezo wetu wenyewe kwenye maeneo hayo kuna hatari ya kudhulumiwa na
kupata hasara. Pengine ipo haja ya kuwa na chombo maalum kwa ajili hiyo
kama tulivyofanya kwa mafanikio kwa upande wa dhahabu.
Changamoto
ya pili ni ile ya kupata Watanzania wengi wenye ujuzi na taaluma
zinazohitajika na soko la ajira la sekta ya gesi. Tusipofanya hivyo
makampuni yataajiri watu hao kutoka nje na hivyo kufanya Watanzania
kutokunufaika na fursa za ajira zilizopo.
Ndugu Wananchi,
Kwa
changamoto hizi mbili, jawabu lipo kwenye elimu na mafunzo tunayotoa
kwa vijana wetu katika shule, vyuo vya ufundi na vyuo vya elimu ya
juu. Kwanza kabisa lazima tuboreshe elimu ya sayansi na hisabati katika
shule zetu za msingi na sekondari. Katika vyuo vya ufundi tutoe
mafundi mchundo wa taaluma zinazohitajika na tasnia ya gesi na
mafuta. Hivyo hivyo kwa upande wa vyuo vikuu nako wafundishe wataalamu
wa fani zinazohitajika kama vile utafutaji wa gesi na mafuta,
uendelezaji wa mafuta na gesi, uchumi na biashara ya mafuta na gesi,
uhasibu na ukaguzi wa mafuta na gesi pamoja na sheria za mafuta na gesi
na mikataba ya utafutaji na uendelezaji wa mafuta na gesi.
Ndugu Wananchi;
Napenda
kuwahakikishia kuwa tayari tumejipanga kutafuta ufumbuzi wa changamoto
hizo. Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinajiandaa kuanza kutoa mafunzo ya Chemical and Environmental Lab for Oil and Gas na fani ya Exploration and Production Software Technologykatika mwaka huu wa masomo. Chuo cha Madini Dodoma kitaanza kutoa mafunzo ya diploma ya Petroleum Geoscience kuanzia
Septemba mwaka huu. Chuo Kikuu cha Dodoma, Chuo cha Sayansi na
Teknolojia cha Nelson Mandela Arusha, na Chuo cha Teknolojia cha Mbeya
na kile cha Dar es Salaam pia wameanza kufundisha mitaala hiyo. Aidha,
VETA Makao Makuu na VETA Mtwara nao wanafundisha masomo yahusuyo
gesi. Wizara ya Nishati na Madini itawadhamini wanafunzi 50 kutoka Mkoa wa Mtwara kwenda kupata mafunzo hayo ya gesi asili katika chuo cha VETA Mtwara.
Ndugu Wananchi;
Wizara
ya Nishati na Madini pia inatekeleza mpango mkakati wa kuwapata
wataalamu wa sekta hiyo kati ya 40-50 kati ya sasa na mwaka 2016.
Taaluma zinazotiliwa mkazo ni Petroleum Geoscience,
Petroleum Geophysics, Petroleum Geochemistry, Petroleum Engineering,
Petroleum Modeling, Oil and Gas economics, Oil and Gas Accounting and
Auditing na Oil and gas Legal Regimes and Contract Negotiations. Kwa
upande wake, Serikali itatoa upendeleo maalum kwa kulipia gharama zote
za mafunzo ili tuweze kuwapata wataalamu hawa mapema iwezekanavyo.
Nawaomba vijana wetu wachangamkie fursa hizi za masomo na watakapohitimu
mafunzo wawe tayari kuitumikia nchi yetu kwa bidii.
Kujenga Uwezo Wetu wa Kutumia Mapato ya Gesi
Ndugu Wananchi,
Changamoto
nyingine kubwa sana ni ile ya kuhakikisha kuwa mapato yatokanayo na
gesi yanatumika vizuri na kwa manufaa ya taifa na watu wake. Lazima
tuanze sasa kufikiria na kujipanga kwa ajili hiyo. Si vyema tukangojea
mpaka hapo mapato yatakapoanza kupatikana ndiyo tufikirie na kutengeneza
mfumo mzuri wa kusimamia na kutumia mapato yatokanayo na
gesi. Tutakuwa tumechelewa, watu laghai na waovu watakuwa wameanza
kunufaika hivyo watakuwa wagumu kutengeneza mfumo utakaowanyima fursa ya
kuliibia taifa.
Jambo hili ni muhimu sana kufanya kwani ipo
mifano hai ya nchi zenye rasilimali nyingi za mafuta na gesi lakini nchi
na wananchi wake hawanufaiki sawia. Mauzo yanafanyika na fedha nyingi
kupatikana lakini manufaa kwa nchi na watu wake ni madogo au hayapo
kabisa. Wanaonufaika ni viongozi na baadhi ya maofisa wa umma
wanaohusika na usimamizi wa shughuli zihusuzo rasilimali hizo. Na, hata
sisi tunaweza kujikuta katika hali hiyo kama tusipojipanga vizuri sasa
ambayo badala ya rasilimali kuwa baraka zinageuka kuwa balaa au hata
laana.
Ndugu Wananchi;
Zipo
nchi duniani ambazo zina usimamizi mzuri wa mapato ya rasilimali za
mafuta na gesi na kuleta baraka na neema kwa taifa na watu wake. Nchi
hizo zimeweza kuhifadhi na kutumia vizuri mapato yake kukuza uchumi wa
nchi kwa jumla na kuboresha upatikanaji wa huduma za kiuchumi na kijamii
kwa watu. Matokeo yake ni watu wa nchi hizo kuishi maisha yaliyo bora
kuliko walivyokuwa kabla ya kupatikana kwa rasilimali hizo. Lakini, hii
imewezekana kutokana na usimamizi mzuri na matumizi mazuri ya mapato
yatokanayo na mafuta na gesi.
Tumeamua kujifunza kutoka nchi za
wenzetu waliofanikiwa ili na sisi tunufaike. Na sisi tunajiandaa
kutengemeza Sera ya Gesi Asili na kurekebisha Sheria ya Utafutaji na
Uzalishaji wa Mafuta na Sheria ya Menejimenti ya Mapato ya Serikali
yatokanayo na gesi zitakazotoa majibu hayo na kuliwezesha taifa kuwa na
mfumo mzuri wa usimamizi wa utafutaji na uchimbaji wa gesi asili pamoja
na usimamizi na matumizi mazuri ya mapato yatokanayo na gesi hiyo. Wapo
wenzetu kwa mfano, wanacho kitu kinachoitwa Sovereign Funds ambapo mapato yote huhifadhiwa na baadae hutolewa kwa utaratibu maalum.
Tunataka tujifunze kutoka kwao ili na sisi tutengeneze chombo chetu cha namna hiyo ili tunufaike.
Ndugu Wananchi;
Mambo
hayo tumeshaanza kuyafanyia kazi. Katika mazungumzo yangu na baadhi ya
wakuu wa nchi rafiki na mashirika ya maendeleo ya kimataifa,
nimewasilisha maombi ya kusaidiwa na kushirikiana kwa mambo
mawili. Kwanza kwa kuwawezesha Watanzania kupata mafunzo ya haraka kwa
wataalamu watakaosaidia kusimamia shughuli za utafutaji, uendelezaji na
biashara ya gesi asili nchini. Pili, watusaidie kupata watu wenye ujuzi
na uzoefu ili watushauri kuhusu namna ya kutengeneza mifumo bora ya
kusimamia na kutumia mapato ya gesi kwa mujibu wa mifano ya wenzetu
waliofanikiwa.
Nafurahi kwamba maombi yetu yamepokelewa vizuri
na nchi zote na mashirika yote ya kimataifa tuliozungumza nao. Baada ya
muda si mrefu kazi itaanza.
Mgomo wa Walimu
Ndugu Wananchi;
Jambo la tatu na la mwisho ni mgomo wa walimu. Pengine
ni mapema kusema kwa vile kesho Mahakama itaamua kuhusu shauri
hilo. Lakini napenda kuwahakikishia walimu kuwa tunawajali,
tunawathamini na kutambua mchango wao muhimu kwa taifa letu. Wakati
wote tumekuwa tunashughulikia madai ya haki zao na malimbikizo
mbalimbali. Madai ya safari hii ni makubwa mno, yametuzidi
kimo. Athari za kuyatimiza yalivyo yataifanya bajeti ya Serikali
kutumia asilimia 75 kwa ajili ya mishahara ya watumishi wa Serikali na kubakiza asilimia 25 kwa
kuendeshea Serikali na kutimiza majukumu ya maendeleo kwa
wananchi. Haitakuwa sawa. Ndiyo maana tumeshindwa kuelewana
walipokataa rai hiyo na wao kusisitiza kugoma.
Wakati
tunaendelea kusubiri uamuzi wa Mahakama, nina maombi mawili kwa
walimu: Moja, wasiwalazimishe walimu wasiotaka kugoma wafanye hivyo,
wawaache waendelee na kazi. Pili, wasitumie watoto isivyostahili
kujenga hoja zao. Nawasihi warudi kwenye meza ya mazungumzo.
Ndugu Wananchi;
Kabla
ya kumaliza hotuba yangu naomba nitumie fursa hii kuwatakia Waislamu
wote nchini kheri na baraka tele kwa swaumu ya mwezi mtukufu wa
Ramadhan. Wakati wote, mjiombee wenyewe kwa Mwenyezi Mungu awajaalie
toba na malipo mema katika mfungo huu. Mkumbuke pia kuiombea nchi yetu
amani, upendo na mafanikio mema.
Baada ya maneno hayo, naomba sasa niishie hapo. Nawashukuru sana kwa kunisikiliza.
Sasa nipo tayari kujibu maswali ya Wahariri kama yapo. Ndugu Wahariri mliopo hapa, karibuni.

Waziri wa Uchukuzi Dkt. Harrison Mwakyembe akielekea ndani ya ukumbo wa Bunge mjini Dodoma Aug,1,2012 kwaajili ya kusoma Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka wa Fedha,2012-2012 (Picha na Mwanakombo Jumaa- MAELEZO).
Waziri wa Nchi , Ofisi ya Rais- Asiye na Wizara Maalumu Prof,
Mark Mwandosya akitoa shukurani Aug,1,2012 kwa Serikali na Wananchi
waliomuombea wakati akiwa mgojwa hadi kupata nafuu na kuweza kuhudhuria
tena katika vikao vya Bunge ,mjini Dodoma. (Picha na Mwanakombo Jumaa-
MAELEZO).
 |
Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Angellah Kairuki akijibu hoja
mbalimbali Bungeni leo kuhusu wizara yake, (Picha na Mwanakombo
Jumaa-MAELEZO). |
Mbunge wa Kigoma Kaskazini Kabwe Zitto (kulia) akitoa maelezo
binafsi kwa waandishi wa habari Aug. 1,2012 kuhusu tuhuma za rushwa
dhidi yake hususan kuelekea katika kupitisha bajeti ya Wizara ya Nishati.
Pichani mwengine ni Prof. Koyela Kahigi (CHADEMA). Picha na Mwanakombo
Jumaa- MAELEZO,
No comments:
Post a Comment