Thursday, January 3, 2013



JESHI la Polisi mkoani Iringa limewafukuza kazi askari Polisi wake wawili G 402 D/C Denis Beatus na F 3277 D/C Karume Farija Kunga baada ya kushiriki katika jaribio la kupokea rushwa.

Askari hao wanadaiwa kupokea rushwa hiyo kutoka kwa ndugu wa watuhumiwa wa pembe za ndovu waliokuwa wakishikiliwa na jeshi hilo tangu Desemba 10, mwaka jana kwa lengo la kupatiwa dhamana.

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), iliwakamata askari hao pamoja na Katibu wa Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali mkoani hapa na kisha kupandishwa kizimbani Desemba 31 mwaka jana kwa tuhuma za kuomba rushwa ya sh milioni sita ili wawasaidie watuhumiwa wa pembe za ndovu.

Watuhumiwa hao walifikishwa mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoa wa Iringa, Consolatha Singano kujibu kesi ya kuomba rushwa ya sh milioni sita kutoka kwa washtakiwa watatu wa nyara za serikali, Abdul Abdallah, Patrick Raymond na Hamsi Solomoni.

Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Imani Mitume, alidai jalada la kesi hiyo namba 306 ya mwaka 2012 lina mashitaka saba.

Alidai kuwa askari namba G 402 D/C Denis Beatus (32) na Joshua Mkwama (37) na Katibu wa Sheria, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Iringa, Joshua Mkama, wanakabiliwa na shitaka la kwanza la kuomba rushwa ya sh milioni sita.

Aliongeza kuwa Beatus anakabiliwa na shitaka la pili la kupokea rushwa hapo Desemba 12 mwaka huu, kutoka kwa Diska Gadama ili kuwasaidia ndugu zake wapate dhamana katika kesi ya kukutwa na nyaraka za serikali kinyume cha sheria.

Mwendesha Mashitaka huyo, alidai kuwa Mkama, anakabiliwa na shtaka la tatu la kupokea rushwa ya sh milioni tatu kutoka kwa Joshua Mkwama katika ofisi ya mwanasheria Desemba 16 mwaka huu.

Kwamba askari namba F 3277 D/C Karume Kunga (32), anakabiliwa na shitaka la nne la kupokea rushwa ya sh. laki tano kutoka kwa Beatus.

Diska Kashinde Gandama mkazi wa Kigamboni Jijini Dar es Salaam ambaye ni ndugu wa washitakiwa watatu wanaokabiliwa na kesi ya kukutwa na nyaraka za serikali, anakabiliwa na shitaka la tano la kutoa rushwa kwa Beatus katika kituo kikuu cha mabasi mkoa wa Iringa.

Shitaka la sita linamkabili Beatus na Gandama ambao wanadaiwa kutoa rushwa ya sh 3,000,000 na kumpa Mkama ili kuwasaidia Patrick na wenzake katika kesi inayowakabili.

Katika shitaka la saba, ilidaiwa kuwa Beatus alimkabidhi Karume Farijala rushwa ya sh laki tano ili kuhujumu kesi dhidi ya nyaraka za serikali inayowakabili watu watatu.

Washtakiwa wote walikana mashitaka na mahakama imeahirisha shauri hilo hadi Januari 15 mwaka 2013.

Washtakiwa wa pembe za ndovu walikamatwa saa 7:45 katika kijiji cha Mtandika, Tarafa ya Ruaha Mbuyuni wilayani Kilolo, Iringa mnamo Desemba 10 mwaka jana wakiwa na pembe za ndovu 78 zilizokadiliwa kuwa na thamani ya sh 934,830,000.

via gazeti la Tanzania Daima


Hatua kuhusu matumizi ya USD milioni 164 za “mabomba ya Mchina”; Mikataba ya miradi ya maji Dar @JJMnyika

Tarehe 3 Januari 2013 kwa kutumia kifungu cha 10 cha sheria ya haki, kinga na madaraka ya Bunge nimetaka Wizara ya Maji inipatie nakala ya ripoti ya utekelezaji wa mradi wa ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya Majisafi na Majitaka Jijini Dar es salaam na maeneo ya Bagamoyo na Kibaha (Dar es salaam Water Supply and Sanitation Project-DWSSP) uliotekelezwa kati ya mwaka 2003 mpaka 2010 jijini Dar es salaam.

Nimetaka ripoti hiyo ili kubaini matumizi ya dola milioni 164.6 zinazoelezwa kutumika katika mradi huo maarufu kama wa ‘mabomba ya mchina’ kwa kuwa mpaka sasa mwaka 2013 sehemu kubwa ya mabomba yaliyowekwa wakati wa mradi huo katika Jiji la Dar es salaam hayatoi maji huku kukiwa na upungufu katika uzalishaji, upotevu wakati wa usafirishaji, udhaifu katika usambazaji na tuhuma za ufisadi katika matumizi.

Pamoja na kutaka ripoti ya utekelezaji wa mradi huo, nimetaka pia nakala ya ripoti ya ukaguzi wa kiufundi (technical Audit) uliofanywa na kampuni ya Howard Humphreys kuhusu mradi huo.

Nimetaka pia kupatiwa ripoti za ukaguzi uliofanywa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa Kampuni ya Maji Dar es salaam- DAWASCO (Dar es salaam Water Supply and Sewerage Company) na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka-DAWASA (Dar es Salaam Water Supply and Sewerage Authority) kwa mwaka miaka mitatu ya 2009/10, 2010/2011, 2011/2012 ili kuweza kufuatilia hatua zinazostahili kuchukuliwa.

Aidha kwa kutumia kifungu hicho hicho cha 10 cha sheria ya haki, kinga na madaraka ya Bunge, katika barua yangu  kwa katibu wa Bunge niliyoiwasilisha leo tarehe 3 Januari 2013 nimetaka kupatiwa nakala za mikataba yote ya miradi inayotekelezwa hivi sasa ya maji katika Jiji la Dar es Salaam ili kuendelea kufanya kazi ya kibunge ya kuishauri na kuisimamia serikali kueupusha kasoro zilizojitokeza katika miradi ya miaka iliyopita kujirudia hivi sasa.

Kati ya mikataba niliyotaka kupatiwa ni ile ya miradi ya miundombinu inayoendelea kujengwa na mikopo iliyopatikana kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu huyo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa  Mpango Maalum wa Maji Dar es salaam 2011-2013 ambao uliwasilishwa katika Baraza la Mawaziri mwezi Machi 2011 na kuridhiwa kutekelezwa ukihitaji jumla ya shilingi bilioni 653.85; ambao utekelezaji wake unasuasua.

Izingatiwe kwamba Jiji la Dar es salaam lina adha ya maji ya muda mrefu ambayo kila mkazi wa jiji hili ana wajibu wa kuhakikisha inapatiwa ufumbuzi hivyo mwaka 2013 utumike kuongeza msukumo wa uwajibikaji katika sekta ya maji ambayo ni muhimu kwa uchumi wa nchi na maisha ya wananchi.

Pamoja na kuwa matokeo ya sensa ya mwaka 2012 kiwilaya na kimikoa bado hayajatangazwa, Jiji la Dar es salaam linakadiriwa kuwa na wakazi zaidi ya milioni nne; hivyo ni sawa na takribani asilimia kumi ya watanzania wote milioni 44.9 waliotangazwa.

Upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es salaam miaka michache baada mwaka 1961 ulikuwa zaidi ya asilimia 68; hivi sasa miaka 51 baada ya uhuru tumerudi nyuma na upatikanaji ni kwa wastani asilimia 55 tu tena kwa mgawo.

Pamoja na kero ya mgawo wa maji hali hii imesababisha ongezeko kubwa la bei ya maji kwa wananchi wa kipato cha chini wanaotegemea kupata maji kutoka sekta binafsi ambapo wanaonunua maji kwa madumu hununua bei ambayo ni takribani mara 15 ya bei ya mteja anayepata huduma ya maji ya bomba.

Hali ni mbaya zaidi kuhusu uondoaji wa maji taka ambapo ni chini ya asilimia 10 tu ya makazi ndiyo yaliyounganishwa katika mtandao wa maji taka na hivyo kuleta uchafuzi wa mazingira hususani katika maeneo yasiyopimwa. Hata katika maeneo yaliyopimwa Jijini Dar es salaam mitandao ya maji taka haijakarabatiwa na kupanuliwa kwa wakati kwa kuzingatia ongezeko la watu suala ambalo lisipochuliwa kwa uzito unaostahili madhara yatatokea katika siku za usoni.

Hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa maji safi na uondoaji wa maji taka zinapaswa kuchukuliwa kuhusu hali hii kwa kuzingatia kuwa idadi ya watu katika Jiji la Dar es salaam inaendelea kukua kwa kasi likiwa ni jiji la tatu kwa ongezeko kubwa la watu barani Afrika na la tisa duniani.

Kwa nyakati mbalimbali katika kipindi cha kati ya mwaka 2000 mpaka 2010 Serikali imekuwa ikitoa ahadi za kumaliza tatizo la majisafi na majitaka katika Jiji la Dar es Salaam bila utekelezaji sahihi, kamili na wa haraka; hivyo uamuzi wa kutumia sheria ya haki, kinga na madaraka ya Bunge na kazi zingine za kibunge nitakazozifanya mwaka huu wa 2013 zitaongeza uwajibikaji katika sekta ya maji kwa manufaa ya wananchi na nchi kwa ujumla.

Imetolewa mtandaoni tarehe 4 Januari 2013 na:

John Mnyika (Mb)

Jimbo la Ubungo

Matajiri 17 KKKT wachanga Bil 1.7/= kuiokoa Corridor Springs Hotel

Mgogoro wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Kaskazini Kati, imeingia katika sura mpya baada ya wafanyabiashara 17 jijini Arusha walioshawishiwa kukubali kuokoa mali za Kanisa hilo zisipigwe mnada.

Taarifa za ndani katika Dayosisi hiyo, zimeeleza kuwa uamuzi wa kushawishi wafanyabiashara hao ambao walikubali kunusuru mali za Kanisa zisipigwe mnada,  ulifikiwa  katika kikao cha dharura cha Halmashauri Kuu ya Dayosisi mwishoni mwa mwaka jana jijini hapa.

Awali kabla ya matajiri hao kuingilia kati, moja ya benki za biashara (jina tunalo) iliipa Dayosisi hiyo muda hadi Desemba 31 mwaka jana, iwe imelipa deni la Sh bilioni 11  vinginevyo mali zake zipigwe mnada.

Kutokana na taarifa hiyo ya benki, Kanisa lilitoa waraka wa Askofu ambapo waumini walitakiwa kila mmoja kuchangia Sh 20,000 ili kunusuru mali za Kanisa zilizo hatarini kufilisiwa mwezi huu baada ya hoteli ya Corridor Springs, mali ya Kanisa hilo kudaiwa fedha hizo.

Baada ya waraka huo, baadhi ya waumini akiwamo Mchungaji Philemon Mollel aliyekuwa kiongozi wa Usharika wa Ngateu, walitaka waliohusika na uzembe uliosababisha deni hilo, wawajibike kabla ya waumini kutoa mchango huo.

Waumini hao walikuwa wakimlenga Katibu Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazani Kati, Israel ole Karyongi, ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya Hoteli ya Corridor Springs, bodi husika na menejimenti kuwajibika.

Hata hivyo, hatua iliyochukuliwa na kuthibitishwa na Karyongi ni kufukuzwa kwa Meneja wa Hoteli hiyo, John Njoroge ili kupisha uchunguzi wa chanzo cha kulimbikizwa kwa deni hilo. Pia Mchungaji Mollel alisimamishwa kazi.

Katika kikao hicho cha Halmashauri Kuu ya Dayosisi, taarifa zilisema ilikubalika iundwe kampuni ya Arusha Lutheran Investment Limited (ALUICO), itakayohodhi mali za Kanisa na iuze hisa kwa wafanyabiashara hao.

Chanzo hicho kilieleza kuwa baada ya kushawishiwa na kugundua thamani ya mali hizo hasa maeneo zinakopatikana kuwa ni kubwa, haraka wafanyabiashara hao walitoa Sh bilioni 1.7 baada ya kila mmoja kutoa Sh milioni 100.

“Kwanza tumeshangaa kuona Kanisa limeamua kufungua kampuni ya kibiashara tofauti na lengo la kuwepo kwake ambako ni kuokoa roho za washarika, hivi tunakwenda wapi? Matajiri hao sasa ndiyo watakaoamua ni kwa namna gani sadaka na zaka za washarika ambazo zilitumika kujenga rasilimali hizo zitakavyotumika, huu ni ufisadi mkubwa kama ufisadi mwingine wowote,” alihoji mtoa habari wetu.

Taarifa zaidi zilisema baadhi ya mali za Dayosisi ambazo hisa zake zimeuzwa kuwa ni pamoja na Hospitali ya Rufaa ya Selian, Corridor Springs, majengo kadhaa yaliyoko jijini hapa na shule za sekondari na ufundi.

“Kila mmoja alioneshwa kupitia kumpyuta katika kikao hicho, mahali mali hizo zilipo na thamani yake na wakashawishiwa kununua kila mmoja hisa zenye thamani ya Sh milioni 100. Kwa kuwa mali hizo nyingi ziko maeneo nyeti kibiashara jijini, wengi walikubali papo hapo na hata wengine waliandika hundi wakiwa bado katika kikao hicho kwa kuwa wana uhakika fedha zao ziko salama au vinginevyo watalazimika kuuziwa mali hizo,” alisema mtoa habari.

Wakati huo huo, kikao hicho kiliamua kumwongeza mkataba wa mwaka mmoja Karyongi baada ya mkataba wake wa awali kwisha Desemba 31 mwaka jana. Karyongi alitafutwa kutoa ufafanuzi lakini simu yake iliita bila majibu.

via HabariLeo



Kushoto ni mwanajeshi huyo akiwa ndani ya gari ya jeshi baada ya kutiwa nguvuni, kulia ni picha alipopiga akiwa na Waheshimiwa wabunge, Lema na Nassari.

Yule mtu aliyedaiwa kuwa ni mwanajeshi wa JWTZ wa kikosi cha Monduli ametiwa mbaroni leo kwa ushirikiano wa jeshi la wananchi na Police.

Uchunguzi wa awali umebaini kuwa kijana huyu hakuwa mwanajeshi wa JWTZ kama alivyojitambulisha kwa waandishi wa habari, ila aliwahi kuwa JKT na akaacha. Amekuwa akivaa ngua hizo za jeshi kwa miaka mingi na wananchi wa Mererani wanamtambua kama mwanajeshi.

chanzo cha taarifa hii: Thechoicetz.com (lakini wavuti.com imeiona taarifa hii awali kwenye Tulonge.com

Wito kutoka Serikalini kwa Watalaamu wa Kitanzania wa ndani na nje ya nchi



KUWATUMIA WATAALAMU WA KITANZANIA WALIOKO UGHAIBUNI (DIASPORA) NA NDANI YA NCHI KUJENGA UWEZO NA UFANISI WA UTEKELEZAJI WA SHUGHULI MUHIMU ZA SERIKALI
______________________________

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inakusudia kuwatumia wataalamu wa Kitanzania walioko ndani ya nchi na wale walioko ughaibuni (Diaspora) katika kutekeleza mipango yake kadhaa yenye umuhimu kwa Taifa.

Hapo awali, Serikali iliwatumia zaidi wataalamu kutoka nchi nyingine, ambapo kwa sasa lengo ni kuona kwamba wataalamu wa nchi nyingine wanatumika pale tu ambapo wataalamu wa Kitanzania walio ndani na nje ya nchi hawajapatikana kufanya kazi husika.

Katika kutekeleza azma hiyo, Serikali itapenda kupata wataalamu wa Kitanzania kwenye maeneo yafuatayo:-

(i)  Mfumo mzima wa utafutaji, uchimbaji, uongezaji thamani na usambazaji wa gesi asilia  na mafuta.

(ii)  Kuimarisha matumizi salama ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika kuboresha utendaji wa Serikali na utoaji wa huduma kwa wananchi.

(iii)  Kuboresha utekelezaji wa malengo ya Serikali na kupima matokeo kupitia mfumo unaokusudiwa kuhakikisha tunapata matokeo  makubwa na ya haraka katika maeneo ya kipaumbele na kimkakati katika maendeleo ya Taifa.

Wataalamu watakaojitokeza na kukubaliwa kufanya kazi Serikalini katika maeneo haya, watafanya kazi kwa mikataba ya muda mfupi, lakini inayoweza kuongezwa iwapo utendaji utaridhisha.

Mwito unatolewa kwa Wataalamu wa Kitanzania popote walipo, ughaibuni au ndani ya nchi, kujitokeza na kuleta wasifu wao (CV’s) pamoja na maelezo ya kwa nini wanafikiri wao ni aina ya watu tunaowatafuta.  Tumia anuani ifuatayo:-

Katibu Mkuu Kiongozi     
Ofisi ya Rais, Ikulu
S.L.P. 9120
DAR ES SALAAM.

E.mail: chief@ikulu.go.tz

No comments:

Post a Comment